Jina langu ni Respicius Luciani Kilambo. Mimi ni Mkristo – yaani mimi ni mtu alyezaliwa upya: Yohana 3:3; Yohana 3:16; Waefeso 2:8-9; Matendo ya Mitume 16:24-31; n.k. Tovuti hii ni matokeo ya mwitikio wa wito wa Bwana Yesu Kristo katika Mathayo 28:19-20 SUV:

28.19  Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu;
28.20  na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari.

Dhima ya tovuti hii ni kumwezesha Mkristo kukua kiroho. Kwa kifupi, kukua kiroho ni mchakato unaofuata baada ya kuzaliwa upya na kujitwalia ile ahadi ya Mungu ya uzima wa milele; hapo kinachofuata ni kujifunza Neno la Mungu (Biblia) na kuliamini; kugeuza maisha yetu yamwelekee Kristo; kupambana na majaribu, mitihani, vishawishi mbalimbali vya duniani; hatimaye kuanza kulitumikia Kanisa la Bwana Yesu Kristo popote pale tulipo kwa kuzitumia karama tunazopewa na Mungu wetu. Tovuti hii haifungamani na dhehebu lolote lile. Lengo lake ni kujua Biblia inafundisha nini na kuyafuata mafundisho hayo, basi! Tovuti hii haina malengo ya kukusanya “sadaka/zaka” kwa namna yoyote ile. Mafundisho yote yaliyomo na yatakayoongezwa baadaye yanatolewa bure; unaweza kuyapakua na kuyasoma kwa wakati wako.

9.27  ... kama vile watu wanavyowekewa kufa mara moja, na baada ya kufa hukumu ...
Waebrania 9:27 SUV

Nakusihi uisikilize ilani hii kutoka kwa Waraka kwa Waebrania katika Neno la Mungu, na ufanye uamuzi muhimu kuliko maamuzi yote katika maisha yako, wa kumwamini Yesu Kristo kwa ajili ya uzima wako wa milele.

Ubarikiwe na karibu!

R. L. Kilambo.